Wednesday, May 19, 2010

Wamechangia, wewe je?

Nimefurahi kuwa leo nimejifunza kitu kipya.

Inaonekana kuwa Vijana wenzetu wako karibu na viongozi wetu. Na cha muhimu zaidi ni kwamba wanajihusisha kwenye shughuli muhimu za siasa -- kampeni na (labda) kupiga kura muda utakapowadia.

Ni jambo jema nadhani; lakini nashindwa kujizuia kufikiria na kujiuliza: Hizi juhudi zingekuwa zinapelekwa kwenye nyanja nyingine muhimu kwenye jamii zetu, mambo si yangekuwa angalau afadhali kulinganisha na hali ilivyo sasa hivi? Mara ngapi umesikia kampeni kama hizi kwa ajili ya kununua madawati au kujenga shule? Au kununua vifaa muhimu kwa ajili ya kuokoa maisha ya watu hospitalini?

Nawaomba chonde chonde jamani Vijana wenzangu mliopata nafasi kama hizi za kuwa "karibu" na viongozi na chama tawala, endeleeni kupiga kelele tunazosikia kwenye nyimbo zenu!

Ukiacha hayo, ingekuwa jambo la busara kama hawa Vijana wenzetu wangetupa sababu za kujihusisha na siasa au chama husika. Kwa mfano: 'Mimi Mwakipesile Albas'tini, nimeamua kujihusisha na kampeni za chama fulani kwasababu zifuatavyo... (a), (b), (c) na (d).' Kuonekana kwenye mabango tu bila kusema chochote inachefua. Je, hizo hela zitatumiwa vipi?

Na mwisho ningependa kutupia jicho suala la Mh. PINDA kutawazwa kuwa kamanda wa VIJANA (CCM) mkoani Rukwa na kaimu kamanda wa VIJANA Taifa, KINGUNGE NGOMBALE MWIRU. Macho yangu yamekuwa kengeza nadhani...

Picha kwa hisani ya Michuzi Jr.

8 comments:

  1. Heri yao kwa kutafuta njia tofauti ya ku'raise party funds. Vyama vingine nchini bado wamekaa siti ya nyuma.

    ReplyDelete
  2. Sisiem noma! Wameshashinda mechi hata kabla gemu halijaanza...

    ReplyDelete
  3. Nimeshukuru kuona SN nawe umeliona hili, pamoja na wadau waliochangia maoni hapa kunitangulia kwani, mimi nami niliona hivi jana, nikawa na maswali mengi kuliko majibu, najiuliza ikiwa kweli ipo nia ya dhati au ni fuata mkumbo, msukumo rika ama hakuna namna ya ku-short cut kuula zaidi ya kwa staili hii, ni mengi nimewaza na kushindwa kuzitumia picha hizi zaidi tu ya kuona zinapendeza machoni na kuwaona wasanii wanaosapoti chama hiki, hilo tu, na hiyo haikujibu maswali yangu mengi.

    Kilichokuwa kikubwa zaidi ni kujiuliza kama vyama vingine vinaona hii na kuchukulia kama changamoto au wanaona aa, faulo, sisi ndo basi tena. Natamani vyama vingine vione hii kama mpambano.

    sigh!

    ReplyDelete
  4. Binafsi, sipingi kile CCM wanachofanya, ila - kama nilivyosema - ningependa kusikia kutoka kwa wahusika nini hasa kilichowafanya kukubali kusaidia chama fulani kwenye kampeni.

    Je, wanakubali "image" yao itumike kama chombo cha kuwahamasisha Vijana kufuatilia na kujishughulisha na Siasa za chama fulani? Bila shaka jibu ni ndio (kwasababu sasa hivi wako kwenye mabango)!

    Lakini ukisikiliza nyimbo za baadhi ya wasanii waliotumiwa utasikia vilio kwa Serikali au viongozi "wanaofanya nao kazi" sasa hivi. Je, wamesahau vilio na kauli zao? Hawa viongozi walizisikia zile nyimbo?

    Kuhusu hii 'tactic'..dah, lazima uwanyooshee mikono Sisiem..Wanatisha kusema ule ukweli. Sasa, kazi ipo kwa vyama vingine.

    Na mwisho kabisa, baada ya kuona haya yote yakitokea mbele yako huna budi kujiuliza, mbona hizi pilikapilika hutokea "mida hii" TU? Nasikia ile barabara ya Mbagala bado haijakamilika, unajua ilianza kutengenezwa lini? Kwa bibi yangu kule hakuna lami...Hospitali nyingi hazina vifaa muhimu. Tumeona picha ngapi kwenye blogs za shule ambazo hazina hata majengo na madawati?

    Lakini, ghafla, wakati wa kampeni hela za kuwasukuma watu wajiandikishe kununua kadi za chama zinapatikana; mahema na masinia ya pilau kila kona.

    Nitaishia hapo...

    ReplyDelete
  5. mimi ningependa tuanze kampeni ya kutafuta hawa watu tuzungumze nao, tuulize hayo maswali ya msingi kama aliyouliza SN. Yaani Professa Jay wa Ndio Mzee..duh!!...

    ReplyDelete
  6. Ukisapoti Sisiem ni ulaji. Jiulize, wale wazee wa Sisiem waliokuwa wanampigia vigelegele JK wakati akiwapiga mkwara wafanyakazi/TUCTA kati yao hawamo wafanyakazi wa zamani wa EAC ambao mpaka leo hii wanadai mishahara?

    ReplyDelete
  7. aah nimeshitushwa na haya mabango,,anywayz labda tuelewe vijana wenzetu wanahitaji kipato na CCM ndio kisima chenyewe...ingependeza kama baada ya huo uchaguzi (which by the way tunajua nani ameshashinda) wafatilie kama ahadi wanazozichangia zitatimizwa,,CCM wamegundua nguvu ya kuwafikia wananchi kupitia wasanii sasa na kama vijana wenzetu wana uchungu na nchi yetu na wamebahatika kupata nafasi basi waitumie kuwa angaza hao viongozi na matendo yao ili watumize ahadi,,.na CCM waelewe tunajua kwamba pesa ya kampeni haitokani na hili changa la macho wanalotupiga

    ReplyDelete
  8. Tukumbuke kuwa wasanii wana uhuru wa kufanya wanachotaka. Ni haki yao... Kwahiyo hatuna haki ya kuwalaumu sana.

    Hii iwe changamoto kwa wengine (vyama vya upinzani).

    Sasa, suala la wasanii kutuambia kwanini wameamua kufanya kazi na chama husika...ni jukumu lao kutuambia au la?

    ReplyDelete