Thursday, May 27, 2010

Tumesahau sakata la Mara?

As-Salaam Alaikum Vijana.

Takribani miezi mitatu iliyopita, blogs zetu zilijaa taswira za wananchi wenzetu walioathirika na uchafuzi wa mazingira - mto Tighithe. Bila shaka macho yako yalishuhudia picha ifuatayo:

Na nina uhakika wengi wetu tulitoa maoni na vilio vyetu. Pia, kuna wale ambao waliahidi kutusaidia kufikisha hili suala kwenye vyombo vya habari vyenye nguvu (Kanada na Marekani). Ni matumaini yangu kuwa zile nguvu, hasira, vilio, mayowe, machozi n.k. hazikuishia kwenye majabali.

Kwa bahati mbaya au nzuri, Vijana FM ilifanikiwa kupata nakala za mikutano na ripoti za mambo yaliyokuwa yanaendelea (kuanzia Mei 2009 hadi mwanzoni mwa mwaka 2010). Binafsi, nadhani kitu muhimu zaidi kilikuwa ni ripoti ya utafiti wa kisayansi uliofanywa na Åsgeir R. Almås, Charles Kweyunga na Mkwabwa LK Manoko.

Sina uhakika watu wangapi walisoma zile makala hapa Vijana FM (tulikuwa ndio kwanza tunaanza...). Uchambuzi wa ripoti za Wizara ya Nishati na Madini unapatikana hapa. Na utafiti uliofanywa na Åsgeir R. Almås et al unapatikana hapa.

Mara ya mwisho niliambiwa kuwa watu wa Foundation HELP waliwapeleka waathirika nane kwenye hospitali ya Muhimbili kwa lengo la kufanyiwa uchunguzi. Mimi sio mtaalamu wa baiolojia, lakini nilitegemea kuwa vitu kama nywele, kucha, n.k. za waathirika zingechukuliwa kwa ajili ya utafiti wa kina -- ambao ungechukua muda mrefu. Na huu ndio ushauri uliotolewa na Åsgeir R. Almås et al.

Lakini, kilichotokea ni hiki: Waathirika walirudishwa kwasababu wanatoka kwenye ukoo mmoja! Kwa maneno mengine, yale yote ni matokeo ya "genetic disorder". Sasa, kipindi chote hiki nilikuwa najiuliza: Hivi, mbona haya matokeo ya genetic disorder yanaonekana baada TU ya uchafuzi wa mto Tighithe?

Chonde chonde wahusika. Sio kila mtu ni mpumbavu... Na Barrick wanajulikana kwa vitendo vyao dunia nzima.

1 comment:

  1. Nadhani mpaka tusikie mamia wameathirika ndio watu watastuka.

    ReplyDelete