Tuesday, April 13, 2010

Watanzania tunaogopa Sayansi?

Takribani miaka miwili iliyopita watu kutoka kila kona ya dunia walikuwa wanazungumzia utafiti wa fizikia uliokuwa unaanza Geneva kutumia Large Hadron Collider (Picha halisi za vifaa na mashine zinazotumiwa zinapatikana hapa (virtual tour)). Ingawa sina takwimu zinazoweza kuniambia ni Watanzania wangapi walikuwa wanafuatilia au kutaka kuelewa nini kilichokuwa kinaendelea, nina uhakika ni wachache sana.

Kwa kifupi, wanasayansi wanataka kutafuta na kuelewa asili ya tungamo (mass); nini hasa hukipa maada uzito?

Maada inajengwa na molecules; ambazo hujengwa na atoms; ambazo zina viini ambavyo vina nucleons (neutrons na protons). Nucleons nazo zina 'vikolombwezo' vyake. "Tatizo" hujitokeza pale unapoangalia tungamo la - kwa mfano - proton moja: proton ina tungamo la 938 MeV/c2 na vitu vitatu (quarks 'uud') vilivyomo ndani ya proton vina jumla ya tungamo la 11 MeV/c2 tu! Na mpaka sasa hivi hakuna ushahidi wa chanzo cha tungamo linalobakia (zaidi ya 925 MeV/c2). Kwa maneno mengine, huo utafiti unaoendelea huko Geneva ni juhudi la kutafuta jibu la hili swali.

Experiments za awali zilikuwa na matatizo ya hapa na pale, lakini wiki mbili zilizopita kulikuwa na mafanikio yaliyokuwa yanategemewa. Na mijadala inaendelea. Lakini katika kipindi chote hiki sikuwahi kuona au kusikia Watanzania wakiwa kwenye midahalo inayohusu huu utafiti na tafisi nyingine muhimu kwa ujumla. Mbona hata hatuulizi maswali? Je, tunadhani haya mambo hayatuathiri kwa njia moja au nyingine? Au hatuna watu wanaoweza kunyambua na kutusaidia kung'amua nini kinachoendelea?

Ifuatayo ni filamu fupi ya Michael Specter ambaye anazungumzia hatari ya jamii kutoipa nafasi sayansi kwa ujumla. Labda baadhi ya mambo ni mapya kwa Watanzania wengi wa kawaida, lakini tujue fika kuwa ndipo dunia inapoelekea. Inabidi tuulize maswali; hata kama huelewi kila kitu kuna uwezekano mkubwa watoto au wadogo zako wakaanza kudunduliza ujuzi wa kuwa wadadisi.



Nimekuwa nikisita kuandika kuhusu mambo kama haya kwasababu hayapewi kipaumbele kwenye jamii yetu kwasababu mbalimbali. Lakini wengi wetu tunajua nafasi gani vizazi vya watoto na wajukuu zetu vitakapokuwa ukilinganisha na wenzao kutoka nchi nyingine.

Kama unadhani mambo haya ni mazito sana, nenda kapumzike halafu rudi hapa kutoa mchango wako!

8 comments:

  1. Aisee mzee this one went over and past my head...nitawaachia wataalamu mgongane vibega, but I will be on the back seat on this one..hahaha

    ReplyDelete
  2. This comment has been removed by the author.

    ReplyDelete
  3. Bahati na wasomaji wengine, sio lazima uwe umebobea sayansi ili uweze kujadili mambo kama haya. Mijadala kama hii mara nyingi huishia kwenye midahalo ya dini vs. sayansi.

    Kwahiyo, nasubiri mchango wako Bahati!

    ReplyDelete
  4. Mkuu sasa tuna jina la Quarks kwa Kiswahili - Vikolombwezo. Itabidi iwe rasmi kuanzia sasa. Anyway, kuhusu Tanzania na sayansi kama ujuavyo nchini Sayansi ni gonjwa la ukoma. Wengi wetu tunaogopa masomo ya sayansi tokea utotoni, sasa itakuwa ngumu pia kwa 'layman' kutaka kujua kuhusu masuala ya sayansi. Cha kushangaza 'layman' huyo huyo anaenda hospitalini, nyumbani anatumia rimoti kubadili chaneli, na anatuma sms kila kukicha. Je anapenda kufahamu how those things work? Je, kuhusu LHC experiment?

    ReplyDelete
  5. Sidhani 'vikolombwezo' ni tafsiri sahihi ya quarks. Lakini ukisoma makala za quarks "up, down, charm, strange, top, bottom", tafsiri haitakuwa mbali sana. Nilikuwa najaribu kuwapa picha wasomaji tu.

    Unadhani mwanafunzi wa kawaida wa fizikia au kemia ya kidato cha pili au tatu anapaswa kujua mtiririko huu: molecules, atoms, nucleons...? Na wale waliofika hadi vyuo vikuu je? Sasa, mbona hata blogs zetu hazitupi taarifa za tafiti muhimu?

    Nina swali lingine kwa wasomaji: Huu ulikuwa ni mwanzo ('kipima joto') tu; je, niendelee kuandika makala kama hizi au nitakuwa najipotezea muda tu?

    ReplyDelete
  6. Endelea kuandika tu. It is refreshing to read science in Swahili

    ReplyDelete
  7. Nimefurahishwa na hii post na sasa ni mda muafaka na sisi tukaanza kuonekana tafadhali naomba msichoke kutupa taarifa kwani sasa Tanzania inaamka kwani kuna Young Earth Scientistic ambayo imekuja kuleta mabadiliko.

    ReplyDelete
  8. Unawetanzania - asante kwa kuja Vijana FM na mchango wako! Inatia moyo...

    Na nimeperuzi blog yako; ingawa mimi siko kwenye field ya Astronomy, huwa napenda kujua kinachoendelea. Nadhani lazima nitaitaja blog yako kwenye makala zangu zinazofuata.

    ReplyDelete